Milipuko miwili ya kujitolea mhanga na mapigano yaliyojiri leo mashariki mwa Libya yameuwa wanajeshi saba na kujeruhi watu wengine karibu ya 50. Wanis Bukhamada, Kamanda wa kikosi maalumu cha jeshi la Libya katika mji wa Benghazi ametangaza kuwa milipuko miwili iliyosababishwa na mabomu mawili ya kutegwa garini katika kituo kimoja cha upekuzi cha jeshi karibu na uwanja wa ndege wa mji huo imeua wanajeshi watatu. Wanajeshi wengine wanne wameuawa katika mapigano kati yao na watu wenye silaha katika mji huo. Kikosi maalumu cha jeshi na wapiganaji wa Khalifa Haftar, Jenerali wa zamani huko Benghazi wanapigana vita na watu wanaobeba silaha likiwemo kundi la Ansarul-sharia. Marekani inalithumu kundi la Ansarul-sharia kuwa lilihusika na shambulio la Septemba mwaka juzi katika ubalozi mdogo wake huko mjini Benghazi, lililosababisha kuuliwa balozi wa Marekani nchini humo. Watu wenye silaha hivi sasa wanavishikilia vituo vya kijeshi vya mji huo wa bandari, huku vikosi vya jeshi la Libya vikiudhibiti hivi karibuni uwanja wa ndege wa mji huo wa Benghazi.
0 toamaon yako: