Babake mtoto wa kipalestina
aliyechomwa moto hadi akafa juma lililopita na walowezi wa kiyahudi
katika maeneo yaliyokaliwa ya ukingo wa magharibi (West Bank) ameaga
dunia.
Sa'ad Dawabsheh ameaga dunia katika hospitali ya Soroka iliyoko Israeli.

Bwana Dawabsheh alipelekwa Israeli ilikupata matibabu baada ya kuungua katika shambulizi
lililoteketeza mtoto wake mchanga wa mwaka mmoja u nusu.
Shambulizi hilo lililotekelezwa na walowezi wa Kiyahudi lilimuacha bwana Dawabsheh mke wake na mwana wao mwenye umri wa miaka 4 wakiuguza majereha mabaya.
Mke wake bi Riham na mwana wao Ahmad bado wako katika hali mahututi.

Shambulizi hilo lililotokea mwisho wa mwezi Julai liliibua hasira miongoni mwa Wapalestina na wanaharakati wa kupigania haki za kibinadamu ambao waliilaumu Israeli kwa kukosa kuwajibikia
usalama wa Wapalestina mikononi mwa Walowezi wa kiyahudi.
Wakati wa shambulizi hilo,Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Ban Ki moon alitaka wale waliohusika kwenye shambulizi la kumchoma mtoto Mpalestina katika eneo linalokaliwa na Israel la ukingo wa magharibi kufikishwa mbele ya sheria.

Waziri mkuu wa Israel Benjamin aliahidi kuwa wale waliotekeleza kitendo hicho alichokitaja kuwa cha kigaidi wangechukuliwa hatua za kisheria.
Netanyahu alielezea mshangao wake kutokana ni kile alichokitaja kuwa mauaji ya kikatili alipowatembelea wazazi wa mtoto huyo na nduguye hospitalini.
Afisa wa Palestina, Ghassan Daghlas, alisema walowezi wa Israil, walichoma moto nyumba nyengine katika kijiji cha Duma hii leo, lakini hakuna mtu aliyeumia vibaya.
Umoja wa Mataifa unasema walowezi wa Israil wamefanya mashambulio kama 120 mwaka huu, katika Ufukwe wa Magharibi uliokaliwa.
0 toamaon yako: