Tanzania swahili radio

IQRA FM RADIO

IQRA FM RADIO
IQRA FM RADIO ELIMU NA MATENDO UIMARA WA RADIO IQRA UPO MIKONOMI MWAKO CHANGIA RADIO IQRA KWA MPESA 0762118805TIGO PESA 0658118804

Sunday, September 28

UISLAM 3-5

Posted by mkachu  |  Tagged as:


Ulimwengu wa Kiislamu Fursa na Changamoto (3)


Sehemu ya tatu ya makala ya Ulimwengu wa Kiislamu, Fursa na Changamoto itaendelea kutupia jicho baadhi ya changamoto na sababu zilizozikwamisha nchi za Kiislamu na kuzifanya zisiwe na mitazamo na misimamo mimoja.
Miongoni wa matatizo makubwa yanayoukabili ulimwengu wa Kiislamu hii leo, ni kutokuweko umoja, mshikamano na mitazamo ya pamoja ya kisiasa baina ya nchi za Kiislamu. Kwa hakika suala hilo huenda likawa limesababishwa na sababu mbalimbali.
Mosi ni kuwa, serikali nyingi zinazotawala katika nchi za Kiislamu zinaamini kwamba, kwa kuzingatia hali ya kiuchumi na kiteknolojia, na muhimu kuliko yote uwezo wa kijeshi wa Magharibi, maslahi na manufaa yao yanaweza tu kudhaminiwa kwa serikali zao kuwa na uhusiano na nchi za Magharibi. Katika upande mwingine, hali ya kulegalega kisiasa na matatizo ya vita vya ndani pamoja na vitisho vya kieneo katika baadhi ya nchi ni mambo yaliyoziongezea nchi hizo hasa watawala wake woga na kuhisi kutokuwa na amani.
Ni kutokana na sababu hiyo ndio maana nchi hizo zikaamua kuwatumia Wamagharibi ili kulinda nafasi zao, kiasi kwamba, baadhi ya nchi hizo zinayategemea madola hayo katika kukidhi mahitaji ya chakula, silaha na hata usalama wao. Leo hii nchi zinazoendelea zimekuwa zikitenga bajeti kubwa ya kununulia silaha na zana za kivita kutoka kwa madola makubwa.
Na ndio maana nchi za Mashariki ya Kati leo hii zikahesabiwa kuwa wanunuzi wakubwa wa silaha duniani. Katika kipindi cha vita vya kichokozi vya Iraq dhidi Iran na Kuwait, takribani dola bilioni 200 za Kimarekani za akiba ya fedha za kigeni za nchi za eneo kama Iraq, Kuwait na Saudi Arabia zilitumika kununulia silaha na zana za kivita kutoka kwa madola ya Magharibi. Hofu ya mashinikizo ya nchi zenye nguvu na satua za madola ya Magharibi na vitisho vyao vya kuziwekea nchi nyingine vikwazo vya kiuchumi na kifedha ni mambo mengine yaliyozifanya nchi za Kiislamu kutokuwa na hamu ya kuanzisha uhusiano baina yao na kutiliana saini mikataba ya ushirikiano. Hussein Abul Fadhli mwandishi wa kitabu cha Mitazamo ya Pamoja ya Ulimwengu wa Kiislamu anaamini kwamba, rasilimali ya kimaanawi huifanya nchi fulani kuwa na nguvu kazi yenye fikra madhubuti. Ikiwa wasomi na wanafikra watalelewa katika misingi ya kitamaduni na ustaarabu wao asilia na wakafanya shughuli zao katika fremu ya matukufu na itikadi zao, hapana shaka kuwa, watakuwa wenzo na nguzo muhimu ya desturi na utamaduni huo. Lakini kinyume na hivyo, endapo watajitenga na kuwa mbali na utamaduni, mila na desturi za taifa lao na wakawa na matatizo ya utambulisho wao ni wazi kuwa, watapelekea jamii yao nayo kukumbwa na matatizo hayo.
Tukichunguza nafasi na mchango wa wanafikra waliolelewa katika mifumo ya kisekula katika kufungamana nchi zinazoendelea na Magharibi, tunaupata kuwa nao si mdogo. Wasomi hao wa Magharibi bila kwanza ya kuwa na uelewa sahihi wa mapungufu na kasoro pamoja mazuri na mabaya ya ustaarabu wa Magharibi wamekuwa wakifuata kibubusa mifumo ya maisha ya Magharibi na kuifanya mifumo hiyo kuwa, kioo na kiigizo chao katika ufumbuzi wa matatizo yao.
Natija ya kuiga na kufuata mfumo huo ni kushindwa na kutokuwa na utambulisho huru. Mbali na matatizo ya ndani, tukitazama kwa makini tunaona kuwa, kuna matatizo na sababu za nje pia zilizopelekea nchi za Kiislamu kubaki nyuma katika masuala mbalimbali. Ukoloni wa moja kwa moja na usikokuwa wa moja kwa moja katika jamii za Kiislamu ulikuwa na nafasi muhimu katika kudhoofisha imani na tamaduni za Kiislamu.
Kuenea kwa mbegu za chuki baina ya kaumu na jamii mbalimbali za Kiislamu ni sababu nyingine iliyopelekea mori, moyo wa izzah na ile hali ya kupigania kujitawala na kujiamulia mambo ipungue katika nyoyo za jamii za wananchi hao. Waislamu ambao kwa makumi ya karne walikuwa waking'ara katika elimu mbalimbali, hivi sasa wanaonekana kubaki nyuma kutokana na njama za wakoloni na hali hiyo inazidi kushuhudiwa kila uchao kutokana na nchi za Kiislamu kuwa tegemezi kwa Wamagharibi. Leo hii kwa kuanzishwa hiki kinachoitwa utandawazi inaonekana kwamba, madola yenye nguvu duniani, yanataka kuutawala na kuudhibiti zaidi ulimwengu lakini kwa mbinu na mtindo mpya. Katika mazingira kama hayo, hapana shaka kuwa, nchi za ulimwengu wa tatu zikwemo nchi za Kiislamu zinakabiliwa na changamoto nyingi.
Kwa mfano, kuwepo kwa utandawazi wa kiutamaduni kutaishia kwa kutawaliwa nchi zote na utamaduni wa Magharibi ambao ni wa mambo na masuala ya kimaada na isirafu katika matumizi. Hasa kwa kuzingatia kwamba, utamaduni wa Magharibi ni wa kutangaza na kueneza vitu vya anasa na vinavyoonekana kuwa ni vya kisasa katika kila pembe ya dunia. Na hasa kwa kutilia maanani kuwa, nembo na vielelezo vya utamaduni wa Magharibi kama vile sinema, intaneti, video, matangazo ya mitindo ya mavazi ambazo vimetawala kwenye mtandao wa vyombo vya mawasiliano duniani, hazitoi fursa ya uwiano wa kubadilishana utamaduni baina ya ulimwengu wa Magharibi na nchi nyingine.
Katika uwanja huo, baadhi ya wakosoaji wa utandawazi wanasema kuwa, mwenendo huo ni mtindo mpya wa ubeberu wa kiutamaduni. Edward Said mhadhiri wa Vyuo Vikuu nchini Marekani mwenye asili ya Palestina anaamini kwamba, Wamagharibi kwa kutumia satua kwa mara nyingine tena wanafanya njama za kuukoloni kiutamaduni ulimwengu wakitumia utamaduni wao. Makala zetu zijazo zitaanza kuchunguza njia za kujiondoa na kujikwamua katika matatizo hayo. Kwa leo tunaishia hapa. Wasalaam Alaykum Warahmatullah Wabarakatuh

Ulimwengu wa Kiislamu Fursa na Changamoto (4) 

Miongoni mwa sifa za ubeberu wa kiutamaduni ni kueneza thamani za mfumo wa ubeberu kama vile namna ya matumizi, mavazi, uhusiano wa kijinsia, haki za binadamu na usekulari au mfumo wa kukana nafasi ya dini katika mfumo wa kisiasa. Kwa utaratibu huo, utandawazi unatoa utamabulisho mpya katika uwanja wa utamaduni, ambao kimsingi unaambatana na kupotea na kuangamia kwa utamaduni na ustaarabu asili wa nchi husika. Jamii za Kiislamu nazo zimekuwa wahanga wa kadhia hiyo. Katika uwanja wa kiuchumi, utandawazi pia unaweza kudhoofisha muundo wa ndani wa kiuchumi wa mataifa ya Kiislamu na kupelekea kuporwa maliasili na utajiri wa nchi hizo. Uchumi wa asili wa jamii hizo unaweza kukabiliwa na matatizo makubwa na ya kimsingi ya utandawazi kupitia mashirika ya kimataifa na taasisi kama Shirika la Biashara Duniani WTO na mengineyo.
Hasa kwa kuzingatia kwamba, nchi hizo hazina suhula za kutosha na muundo wao wa kiuchumi hauna uwezo wa kushindana na madola makubwa na yenye nguvu kiuchumi duniani. Ama kwa upande wa kisiasa, kutokea mihimili mipya yenye nguvu duniani kama vile mashirika na makundi ya kimataifa hasa vyombo vya mawasiliano kama vile Intaneti, satalaiti na mitandao mingi ya vyombo vya habari kumepelekea kulegalega kwa mipaka ya kitaifa. Cha kusikitisha zaidi ni kuwa, asasi za kimataifa kama Umoja wa Mataifa wakati mwingine zimekuwa zikitumiwa kama wenzo wa madola makubwa kwa ajili ya kutekeleza matakwa ya madola hayo.
Ibn Khaldun alimu na mwanazuoni mkubwa wa Kiislamu, anazungumzia sababu muhimu za maendeleo katika jamii akisema, mambo mawili ni muhimu kwa ajili ya maendeleo. Mosi, kiongozi muadilifu na pili ni kuungana kwa jamii au kwa taifa na taifa jingine. Kuhusiana na suala hilo, leo hii baadhi ya wanafikra wamefikia natija hii kwamba, kutokuwepo tawala za kiadilifu na kukosekana moyo wa kuwaunganisha pamoja watu na kushirikiana pamoja ni miongoni mwa sababu zilizozifanya nchi nyingi kubaki nyuma kimaendeleo.
Mazingira yanayotawala leo hii ulimwenguni yanazilazimisha tawala kuliko kipindi kingine chochote kile kuwashirikisha wananchi katika nyanja mbalimbali ili ziweze kukabiliana au kutatua matatizo yanayozikabili. Kwa hakika suala hilo ni nguzo muhimu ya kuzihalalisha tawala zilizoko katika nchi mbalimbali ulimwenguni zikwemo nchi za Kiislamu.
Katika kipindi cha miongo mitatu iliyopita, kumetokea matukio tofauti katika masuala mbalimbali ambayo yamepelekea mlingano wa dunia kukumbwa na mabadiliko makubwa. Kutokea mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran, kusambaratika Umoja wa Kisovieti, maendeleo makubwa yaliyopatikana katika uwanja wa teknolojia na mawasiliano, ni miongoni mwa matukio ambayo yaliibadilisha mno sura ya miaka ya mwishoni mwa karne ya 20.
Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran si tu kwamba, yalivuruga mahesabu ya madola ya Maghribi katika eneo muhimu na la kiistratejia la Mashariki ya Kati, bali mapinduzi hayo, adhimu yalikuwa na taathira kubwa kwa Waislamu ulimwenguni kote. Miongoni mwa mabadiliko makubwa yaliyotokea katika ulimwengu wa Kiislamu ni kutokea ufahamu na mwamko mkubwa wa wananchi. Dr Hasan Rahimpour Azghadi, mtafiti wa Kiirani na mhadhiri wa chuo kikuu anasema hivi kuhusiana na suala hilo: "Ufahamu na mwamko huo ambao ni mwamko wa kidini, huenda karne moja iliyopita, ulikuwako katika kundi dogo la wanafikra waliobobea kwenye ulimwengu wa Kiislamu. Lakini leo hii mwamko huo unaonekana kuenea katika uma wote wa Kiislamu." Mtafiti huyo wa Kiirani anaendelea kusema, "mwamko huo hasa katika kipindi cha miaka 100 ya mwisho, umetokea baada ya karne kadhaa za kusalimu amri na kujilegeza mbele ya ukoloni. Leo hii Waislamu wanatambua vyema kwamba, sababu kuu ya kubaki kwao nyuma kiuchumi na kielimu na mifarakano na migawanyiko iliyopo katika ulimwengu wa Kiislamu imetokana na Waislamu kuwa mbali na mafunzo aali ya dini yao tukufu." Mwisho wa kunukuu.
Kutokana na Waislamu kubadilika kuhusiana na matukio mbalimbali yanayowazunguka, leo hii tunaona kuwa, katika ulimwengu wa Kiislamu kumekuwa kukipendekezwa masuala kama ya umoja wa uma wa Kiislamu, kuundwa asasi na jumuia za Kiislamu, ustawi wa kieilmu ambao kimsingi ni maendeleo na ustawi katika uga wa fikra za walimwengu kwenye ulimwengu wa Kiislamu.
Suala hilo limeyafanya madola ya Kiislamu kufahamu kwamba, leo hii matakwa ya wananchi yana daraja ya juu zaidi kuliko mahitaji yao ya kila siku. Hata wito wa mabadiliko ya kisiasa wa Magharibi au mapendekezo yao ya demokrasia ulimwenguni hasa katika Mashariki ya Kati, ni masuala yanayotokana na kudhihiri mabadiliko ya kifikra katika ulimwengu wa Kiislamu. Hapana shaka kuwa, madola ya Magharibi kamwe hayazingatii matakwa ya wananchi wa mataifa ya Kiislamu, bali yanajaribu kuzipotosha fikra za waliowengi kwa kutanguliza mbele matakwa ya wananchi hao, kumbe wanataka kufikia malengo yao haramu ili kwa njia hiyo waweze kudhibiti hali ya mambo katika eneo na matukio ya ulimwengu wa Kiislamu. Mashambulio ya Marekani na washirika wake dhidi ya Iraq yalifanywa kwa kisingizio cha kuwaletea demokrasia wananchi wa nchi hiyo, lakini wavamizi hao hawajawaletea chochote wananchi hao ghairi ya machafuko na mauaji. Hii ni katika hali ambayo, Marekani ilikuwa ikimuunga mkono kijeshi, kisiasa na kiuchumi dikteta wa zamani wa Iraq Saddam Hussein.
Mpenzi msomaji na mfuatiliaji wa makala hizi za Ulimwengu wa Kiislamu, Fursa na Changamoto, sehemu ya nne ya makala yetu inaishia hapa. Sehemu ijayo ya makala hii mbali na kuzungumzia umuhimu wa kuweko kambi moja au mtazamo mmoja katika ulimwengu wa Kiislamu kwa ajili ya kukabiliana na changamoto unazozikabili, itatupia jicho pia uwezo na suhula zilizoko katika nchi za Kiislamu. Wassaalam Alaykum Warahmatullah Wabarakatuh.

Ulimwengu wa Kiislamu Fursa na Changamoto (5) 

Miongoni mwa maudhui ambazo katika kipindi cha miongo miwili iliyopita zimekuwa zikijadiliwa na hasa baada ya kusambaratika Umoja wa Kisovieti katika uga wa mfumo wa kimataifa, ni suala la kuwa na kambi yenye mitazamo ya pamoja.
Nchi ambazo katika zama hizo zilijiunga na kambi zenye nguvu ili kulinda na kuhifadhi maslahi yao, leo hii kwa kuanzisha taasisi kama Umoja wa Ulaya, Muungano wa Nchi za Mashariki ya Asia ya Kusini ASEAN na kadhalika, zinafanya jitihada za kuimarisha nguvu, satua na nafasi zao kimataifa. Hata hivyo, cha kusikitisha ni kuwa, nchi za Kiislamu licha ya kuwa katika eneo muhimu kijiografia na kistratejia na kuwa na suhula nyingi ukiwemo utajiri wa nishati ya mafuta, hazijastafidi ipasavyo na suhula hizo. Kwa mfano katika hali ambayo, nishati ni chanzo kikubwa kabisa cha pato la fedha za kigeni duniani na asilimia 75 ya akiba ya mafuta na gesi duniani, inapatikana katika nchi za Kiislamu; lakini cha kusikitisha ni kwamba, nchi hizo hazijastafidi kwa njia sahihi na utajiri huo.
Leo hii kwa kuzingatia mazingira yanayotawala ulimwenguni, udharura wa kuweko kambi yenye misimamo mimoja na ambayo itashirikiana katika ulimwengu wa Kiislamu kuhusiana na masuala mbalimbali ulimwenguni unahisika zaidi kuliko kipindi kingine chochote kile. Hasa kwa kuzingatia kwamba, madola ya Magharibi yamezidisha hujuma, njama na propaganda zao dhidi ya nchi za Kiislamu.
Hapana shaka kuwa, kudhalilishwa na kuvunjiwa heshima matukufu na itikadi za Kiislamu katika vyombo vya Magharibi na mashambulio ya kijeshi ya Marekani na kisha kuendelea kuweko kijeshi Washington katika ardhi za Kiislamu za Afghanistan na Iraq au mashambulio ya kijeshi ya utawala dhalimu wa Israel dhidi ya Lebanon na jinai za utawala huo kwa wananchi madhulumu wa Palestina ni mifano ya wazi ya njama za hujuma za dhahiri dhidi ya ulimwengu wa Kiislamu. Ni kwa kuzingatia hayo ndio maana leo hii suala la umoja, mshikamano na nchi za Kiislamu kuwa na kambi na mitazamo ya pamoja baina yao yakawa mambo ambayo yana umuhimu mkubwa kuliko kipindi kingine chochote kile. Ni jambo lisilo na shaka kuwa, kuna uwanja na mazingira mazuri kwa nchi za Kiislamu kuwa na kambi moja na yenye misimamo na mitazamo mimoja katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kielimu.
Miongo kadhaa iliyopita, istilahi ya mtazamo mmoja ilikuwa ikitumiwa mno katika matini za kisiasa. Baada ya Vita Vikuu vya Pili vya Dunia istilahi ya mtazamo wa pamoja ilianza kuzingatiwa mno na nchi mbalimbali duniani. Katika uwanja huo, nchi za Ulaya Magharibi zililipa kipaumbele suala la mtazamo wa pamoja wa kieneo katika siasa na mipango yao. Soko la pamoja na kubadilishwa kwake kuwa Umoja wa Ulaya ni natija ya jitihada za nchi za Ulaya katika uwanja huo.
Kumalizika vita baridi na kusambaratika Umoja wa Sovieti kulipelekea kutokea mabadiliko makubwa na muhimu katika muundo wa mfumo wa kimataifa na muhimu kuliko yote ni mabadiliko ya kambi mbili na ni katika kipindi hicho pia ambapo Marekani ilianza jitihada za kuanzisha mfumo wa dola moja lenye nguvu.
Leo hii kutokana na hali mpya ya hivi sasa, nchi nyingi zinazingatia suala la mtazamo mmoja wa kieneo au kambi moja ya kisiasa, kiuchumi na kadhalika ya kieneo kuwa, moja ya njia bora za kukabiliana na mfumo wa dola moja lenye nguvu wa Marekani. Kumejitokeza mitazamo mbalimbali au kambi tofauti za kieneo katika sekta mbalimbali. Mtazamo wa pamoja katika uhusiano wa kimataifa ni nadharia ambayo nchi zinafanya jitihada za kushirikiana katika masuala mbalimbali kwa mujibu wa maslahi yao ya pamoja. Hadi sasa mikataba kadhaa imetiwa saini katika fremu ya ushirikiano wa kiuchumi na kisiasa. Mazingira yanayotawala leo hii duniani kwa upande mmoja na hali ya mambo katika ulimwengu wa Kiislamu kwa upande wa pili, ni mambo yanayozifanya nchi za Kiislamu kuchukua hatua za kushirkiana zaidi. Nchi za Kiislamu zina mambo mengi yanayoshabiana kama vile dini, utamaduni, na kuwa na mipaka ya pamoja, na kuwa na suhula na fursa zinazofanana za kiuchumi, ni mambo ambayo kwa hakika yanaziandalia uwanja mzuri nchi hizo, wa kuwa na mitazamo mimoja katika masuala mbalimbali, hasa kwa kuzingatia kuongezeka
hivi sasa njama za maadui wa Uislamu katika pembe mbalimbali duniani. Pendekezo la kuweko na mtazamo mmoja na umoja katika istilahi za kisiasa kwenye ulimwengu wa Kiislamu linarejea nyuma kabla ya karne moja. Kwa hakika kuna mambo na sababu nyingi za ndani na za nje zilizowafanya wanaopenda umoja katika ulimwengu wa Kiislamu kuona kuwa kuna udharura wa kuweko na mtazamo na msimamo mmoja. Vitu kama dini na utamaduni wa pamoja na tajiriba ya nchi zote za Kiislamu zilioipata kutokana na kukoloniwa, hasa hatua ya Wazayuni ya kuzikalia kwa mabavu ardhi za Wapalestina, bila shaka ni mazingira ya kiutamaduni na kisiasa yanayoziandalia uwanja nchi za Kiislamu kuwa na mtazamo mmoja.
Kwa upande wa nafasi ya kijiografia, kiistratejia na uwezo wa kiuchumi, nchi za Kiislamu zina mazingira mazuri na mwafaka ya kushirikiana na kuwa na misimamo ya pamoja. Licha ya kuwa na mambo mengi yanayoziandalia mazingira mazuri nchi za Kiislamu ya kushirikiana na kuwa na mitazamo ya pamoja, lakini watafiti wa Ulimwengu wa Kiislamu wanasema kuwa, Uislamu na utamaduni mkongwe wa nchi hizo ni mambo muhimu kabisa yanayoziandalia uwanja nchi hizo kushirikiana na kuwa na mitazamo pamoja na malengo mamoja. 

 

0 toamaon yako:

Author

CONTACT ME FOR WEB AND BLOG DESIGNING...

uislam na maisha yake

uzayuni

swahili radio

uislam na maisha

mohamed waziri

Subscribe to our Mailing List

We'll never share your Email address.
+255 (762) 118-805 mohamedwaziri295@gmail.com